Wednesday, April 29, 2009

MILIPUKO YA MABOMU KATIKA PICHA


Muuguzi wa hospitali ya Temeke akiwa amembeba mmoja wa majeruhi wa milipuko ya mabomu


Mabaki ya bomu likiwa limetua katika matofali pembezoni mwa nyumba


Wakazi wa Mbagala wakiyahama makazi yao kwa muda baada ya milipuko ya mabomu


Majeruhi wa milipuko ya mabomu wakipatiwa huduma ya kwanza katika hospitali ya Temeke


Askari wa JWTZ akiwa amebeba moja ya mabaki ya milipuko ya mabomu

MABOMU YATIKISA DAR

Milipuko ya mabomu yaliyokuwa yamehafadhiwa katika ghala la kutunzia silaha hizo ya Kambi ya Jeshi ya Mbagala Kizuiani imelitikisa jiji la Dar mapema aubuhi leo na kuendelea mpaka nyakati za mchana.

Mwana 'Sponsor' ambaye alikuwepo eneo la tukio alishuhudia wakazi wa maeneo hayo wakiyahama makazi yao kutokana na hofu kubwa iliyokuwa imetanda miongoni mwao. "Nilikuwa nimekaa chini hapa, ghafla nikasikia mlipuko mkubwa ambao sikuwahi kuusikia tangu nizaliwe." Alisema Mkazi mmoja wa eneo hilo.

Sponsor ilishuhudia vikosi mbalimbali vya ulinzi vya jeshi la Wananchi vikiwa katika eneo hilo kulinda usalama wa wananchi, na kuhakikisha wanadhibiti milipuko hiyo. "Haya mabomu ni kama mfano wa 'missile' (makombora), yanapolipuka husafiri umbali wa zaidi kilometa 10." Alisema mmoja wa askari wa JWTZ.

Katika Hospitali ya wilaya ya Temeke, hali ilikuwa ni ya majonzi baada ya hospitali hiyo kufurika majeruhi wa milipuko hiyowaliokuwa wamelala sakafuni na wengine wakionekana kupoteza fahamu kabisa.

Idadi kubwa ya majeruhi hao ni wanafunzi wa shule za Msingi na Sekondari, wengi wao wakiwa ni wasichana. Sponsor pia ilishuhudia wauguzi wa hospitali hiyo wakitoa huduma ya kwanza ambao walikuwa wakipigana vikumbo katika kordo za hospitali kwa kupokea miili ya majeruhi.

Ndugu na jamaa wa karibu wa majeruhi hao walionekana kutokwa na machozi, huku wengine kuchanganyikiwa wakiwa wanapepea majeruhi hao hospitalini hapo. Mpaka sponsor inakwenda mitambo, idadi ya majeruhi wa milipuko hiyo haikujulikana.


WAnajeshi wakilundika mabaki ya mabomu yaliyolipuka

Tuesday, April 28, 2009

JK azindua Angaza Zaidi


Rais Jakaya Kikwete akibonyeza kitufe kuzindua mradi wa Ushauri Nasaha na Upimaji wa vvu, (Angaza Zaidi), leo jijini


Waigizaji wa kundi maarufu la Vichekesho nchini 'Orijino Komedi' wakifanya vitu vyao wakati wa uzinduzi huo leo

Monday, April 27, 2009

Kabuye aagwa

Mwili wa aliyekuwa mbunge machachari katika bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Phares Kabuye umeagwa rasmi leo katika hospitali ya Muhimbili Dar es Salaam tayari kwa kusafirishwa kuelekea jimboni kwake, Biharamulo kwa mazishi.

Marehemu Kabuye alifariki juzi kwa ajali ya Basi la Kampuni ya RS wilayani Kilosa, Morogoro na anatarajiwa kuzikwa kesho jimboni kwake.


Baadhi ya waombolezaji na wanachama wa chama cha Tanzania Labour (TLP), wakitoa heshima za mwisho kwa mwili wa marehemu Phares Kabuye, Dar es Salaam leo

Sunday, April 26, 2009

Athari za mvua zinazoendelea kunyesha jijini Dar katika picha..

Mvua zinazoendelea kunyesha jijini hapa zimeendelea kuleta athari mbalimbali kama Sponsor ilivyoshuhudia leo katika maeneo mbalimbali ya jiji hili la Dar. Unaweza kujionea baadhi ya athari hizo kupitia picha hizi..

alt=""id="BLOGGER_PHOTO_ID_5328981882432847938" />
Mkazi wa jijini eneo la Mbagala akijaribu kujinasua katika dimbwi la maji baada ya kuzama kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha

Magari yakipita kandokando ya mtaro uliomong'onyoka na kusababisha kuharibika kwa kipande cha barabara ya Kilwa, eneo la Mbagala Kizuiani leo kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha

Wakazi wa eneo la Mbagala rangi tatu wakipita kwa shida katika moja ya dimbwi lililojaa maji machafu kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha jijini hapa

Mrema awazuia Mutungirehi na Kinanda kuingia Mkutanoni

Katika hali inayooonyesha demokrasia kwa baadhi ya vyama vya siasa nchini kutokukomaa, Mwenyekiti wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Lyatonga Mrema amewatimu wagombea wa nafasi za uongozi wa juu katika chama hicho katika mkutanoni mkuu wa taifa wa uchaguzi wa chama hicho, Joram Kinanda na Mutungirehi leo jijini hapa.

Wakiwa wamesimama nje ya ukumbi wa mkutano huo wagombea hao wameiambia Sponsor kuwa awali walipewa mwaliko wa kuhudhuria Mkutano huo na Mwenyekiti wao, Mrema lakini wameshangaa hatua ya kuzuiwa kuingia mkutanoni muda mfupi baada ya kuwasili.

Kwa upande wake, Mrema amesema kuwa wagombea hao wamevamia mkutano huo pasipo kualikwa jambo lililopelekea kuwazuia wasiingie mkutanoni kwa kuhofia wangeleta vurugu kubwa kutokana na tofauti zilizopo baina ya wagombea hao na Mrema.

Mkutano Mkuu wa Taifa wa Uchaguzi wa TLP unaendelea kufanyika leo, katika ukumbi wa Milleium huko Mbagala, wilayani Temeke ambapo wajumbe na wanachama wa chama hicho watapiga kura kuchagua viongozi wapya.


Wagombea wa nafasi za juu za Uongozi wa chama cha TLP, Joram Kinanda (kushoto) na Mutungirehi wakijadili jambo sambamba na wafuasi wao muda mfupi baada ya kuzuiwa kuingia mkutanoni

Friday, April 24, 2009

Walemavu wakiwezeshwa wanaweza..

BENKI ya Standard Chartered leo imetoa msaada wa kompyuta tatu kwa chama cha wasioona Tanzania (TLB), kupitia Shirika la Kimataifa la Wasioona (Sightsaver International) ikiwa ni moja ya malengo ya benki hiyo hapa nchini kusaidia jamii katika upande wa elimu.

Akizungumza na wahabarishaji katika makao makuu ya Shirika hilo, yaliyopo Mikocheni jijini hapa, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano cha benki ya Standard Chartered, Lucy Kihwele amesema kuwa msaada huo wa kompyuta utakuwa ni changamoto kwa wahisani ndani na nje ya nchi kuwa walemavu ni wanajamii ka zilivyo jamii nyingine na pia wakiwezeshwa wataweza.

Alisema kuwa benki yake imedhamiria kuwasaidia walemavu nchini katika upande wa elimu na huo ukiwa ni mwanzo tu wa dhamira hiyo.


Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Kimataifa la Kusaidia Wasioona (Sightsavers International), Dkt. Ibrahimu Kabole (kushoto) akionyesha namna kompyuta inavyoweza kutumiwa na mlemavu wa macho..

Wednesday, April 22, 2009

Ufukuaji mbegu DECI ni mbinde usipime...

Wanachama wa iliyokuwa kampuni ya upandaji na uvunaji mbegu (DECI Tanzania Ltd) leo walikusanyika katika ofisi za kampuni hiyo zilizopo Mabibo, jijini kwa ajili ya kufukua mbegu zao ambazo nyingine bado hazijaanza kuota.

Sponsor ilifika eneo la tukio na kukuta maelfu ya wanachama hao wakiwa wameizunguka ofisi ya DECI huku wakisukumana kwa ajili ya kuingia ndani kufukua mbegu zao hizo. Hali haikuwa ya kuridhisha kwani msongamano huo ungeweza kuleta maafa kutokana na kila mmoja wao kutaka kuwa wa kwanza kungia kurudishiwa mbegu zake.

Monday, April 20, 2009

Binua Mchanga linapotumbukia Korongoni


Wakazi wa eneo la Kimara Temboni wakiangalia gari la kubeba mchanga 'binua mchanga' likiwa korongoni baada ya kuacha njia, eneo hilo, leo asubuhi jijini hapa...

Sunday, April 19, 2009

SERIKALI YAPIGILIA MSUMARI WA MWISHO DECI

SERIKALI imesema haiitambui kampuni ya kupanda na kuvuna fedha (DECI Tanzania Limited) kama ni taasisi inayoendesha shughuli zake kihalali.

Akizungumza na waandishi wa habari leo mchana, Waziri wa Fedha na Uchumi Mustafa Mkulo amewaambia waandishi wa habari kuwa Kampuni hiyo ilikujisajili kama shirika moja la kidini la 'Evangelic' kwa ajili ya kutoa huduma za kiroho lakini wameshangaa kuona imejiingiza katika biashara ya upatu.

"Kwanza tangu wameanza kuandikwa katika vyombo vya habari, sijawahi kuona hata sehemu moja iliyoandika kuwa haijasajiliwa na Benki Kuu Tanzania (BoT), Alisema na kuongeza

"Kama serkali tunasema kuwa kampuni hii ilikuwa inaendesha shughuli zake kiujanja ujanja, hivyo hatua kali kwa mujibu wa sheria ya Tanzania itachukuliwa ikiwa ni pamoja na kuwafikisha vingozi wake katika vyombo vya sheria." Alisema.



Waziri Mkulo akizungumza na waandishi wahabari leo

Friday, April 17, 2009

Taswira ya jamii katika Taifa


Wakazi wa eneo la Vituka, Dar es Salaam wakivuka mto Yombo kwa tabu kama walivyonaswa na Sponsor leo mchana. Eneo hilo halina majira ya kiangazi wala masika, maji kukatiza hapo ni desturi ya kawaida, hivyo kuwalazimu wakazi wa eneo hilo na watumiaji kwa ujumla kuvua viatu na kisha kuyakata maji.

Mwalimu awafungia milango wanafunzi kisha alala mbele..

Katika tukio la kushangaza wakazi wa eneo la Yombo Vituka, Dar es Salaam Mwalimu Mkuu wa shule ya sekondari Barabara ya Mwinyi amefunga milango ya madarasa ya shule hiyo na kisha kutembea mbele.

Sponsor ilitembelea eneo hilo na kukuta vurugu kubwa ya wanafunzi hao huku wakiwa wamebeba bango kubwa likiwa linasomeka 'MKUU HATUTAKI UFISADI UONDOKE, BY WANAFUNZI' huku wakipiga mayowe "Hatukutaki uondoke... tumechoka na mateso yakoo.."

Mmoja wa walimu aliekuwepo eneo hilo la tukio aliiambia sponsor kuwa chanzo kikubwa cha vurugu hizo ni Mwalimu Mkuu kuamua kuwafungia milango ya madarasa wanafunzi hao kwa madai ya kushindwa kulipa baadhi ya michango, ambayo hata hivyo wanafunzi hao walidai ni batili na ya kifisadi.

"Anatulipisha shs 5000 wakati tunatakiwa kulipia shs 200, huyu ni fisadi hatumtaki aondokee..." Alisema mmoja wa wanafunzi hao aliejitambulisha kwa jina la Hamis Mbegu, huku akiwa na jazba.

Juhudi za kumpata mwalimu Mkuu huyo aliyefahamika kwa jina la Hellen Mngoya, zilifanikiwa baada ya Sponsor kutafuta namba zake za simu na kisha kumpigia. Baada ya kumpigia simu na kupokea mazungumzo yalikuwa kama ifuatavyo;

Sponsor: Unatuhumiwa na wanafunzi wako kwa ufisadi wa michango na kuwakosesha masomo, unalizungumziaje hili?
Mwalimu: Wewe ni nani kwanza, jitambulishe.
Sponsor: Mwandiishi wa habari, nimekuta vurugu za wanafunzi wako wakidai umewafungia milango ya madarasa kwa sababu unawadai michango, naomba maelezo.
Mwalimu: Mimi nilitoka kwenda kuchukua mitihani, wakati nikiwa nimeshawaruhusu wanafunzi wote. hivyo kilichotokea nyuma sikifahamu.
Sponsor: Wanafunzi wanadai kuwa umewakosesha masomo kwa kuwafungia milango ya madarasa, sababu unawadai michango ambayo wao wanadai ni batili, unasemaje?
Mwalimu: Mimi siwezi kuzungumzia suala hilo, mtafute ofisa elimu ndiye anyejua kila kitu kuhusu shule ile.

Baada ya kumaliza mazungumzo hayo, Sponsor pia ilimtafuta Ofisa elimu wa Wilaya ya Temeke ambaye nae alidai hakuwa na taarifa zozote kuhusiana na vurugu hizo, ingawa ni kweli anafahamu matatizo ya shule hiyo.

Shule hiyo yenye wanafunzi wa kidato cha kwanza mpaka cha tatu ina jumla ya walimu 13, na ni moja ya shule zilizomo katika mpango wa serikali wa shule za kata.



Wanafunzi wa Shule ya Sekodari Barabara ya Mwinyi, kata ya Vituka wakiwa wamebeba bango lenye ujumbe wa kukataa uongozi wa Mwalimu Mkuu wa shule hiyo kama walivyonaswa na Sponsor.

Thursday, April 16, 2009

Lukuvi, angalia baadhi ya changamoto hizi katika picha...


alt=""id="BLOGGER_PHOTO_ID_5325290565167356674" />


alt=""id="BLOGGER_PHOTO_ID_5325290559685672322" />


alt=""id="BLOGGER_PHOTO_ID_5325290553649664738" />


alt=""id="BLOGGER_PHOTO_ID_5325290552743513650" />

Kwa heri Kandoro, karibu Lukuvi na hizi ndizo changamoto zetu..

Aliyekuwa Mkuu wa mkoa huu wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro amehamishiwa mkoani Mwanza kikazi ambapo mikoba yake sasa imechukuliwa na William Lukuvi aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Dodoma. Hapana shaka Kandoro atakumbukwa kwa mengi mema yake aliyoyafanya katika jiji hili lenye changamoto lukuki, akiwa na dhamira ya kujaribu kuhakikisha mambo yanakwenda sawa.

Changamoto ambazo bado zinaukabili mji huu ni nyingi. Lakini zipo zile changamoto kubwa kubwa ambazo ni tatizo la maji, umeme, usafiri, msongamano wa majumba na watu na kadhalika.

Ninavyofahamu mimi, hata angeletwa binadamu wa aina gani kuongoza miji mikubwa kama huu wa Dar es Salaam, bado atakuwa anakabiliwa na changamoto mbalimbali na si kutatua zote kama wengi wetu tunavyodhani. Ni dhahiri shahiri, watanzania tulio wengi tunatamani kuwa na maisha mazuri kwa muda mfupi sana, hilo halina ubishi.

Hivyo inatupasa kumshukuru Kandoro kwa aliyoyatenda katika kipindi cha uongozi wake jijini hapa. Wapo wenzangu watakaomtoa kasoro kulingana na utashi wao, wapo watakaokuwa hawana maoni yoyote wale wenzangu wa 'no comments', na pia wapo ambao wapowapo tu, hata ukiwauliza utamkumbuka Kandoro kwa lipi alilolifanya hapa jijini, wao watakwambia 'kwa mengi tu' halafu ukiwaambia wakutajie hata moja, watakujibu 'sikumbuki'.

Mji huu ni mkubwa, ukilinganisha na mingine. Ninapozungumzia ukubwa namaanisha mzunguko wa hela katika mji huu ni mkubwa sana kutokana na kuwepo kwa vyanzo vingi vya mapato ya Serikali ukilinganisha na miji mingine. Bandari, Reli, Barabara, Uwanja wa ndege, Viwanda, Maduka makubwa, na vinginevyo ni miongoni mwa vyanzo hivi vya mapato ya Serikali yanayofanya mzunguko mkubwa wa hela.

Hivyo basi, kutokana na hayo yote, wananchi wengi hukimbilia mji huu kujitafutia ajira na wengine kujiajiri wenyewe. Mbali na hilo, pia wawekezaji wengi wamekimbilia mji huu kuwekeza kutokana na kuwepo kwa angalau mazingira mazuri ya uwekezaji. Hivyo ni dhahiri kuwa, changamoto katika mji huu si jambo la kulishangaa, bali pia ni sehemu ya maisha katika mji huu.

Hili linanifanya sio tu kumnyooshea kidole Mheshimiwa Kandoro eti 'mbona jambo fulani halijatekelezwa' bali pia kuamini binadamu sisi kamwe hatuwezi kulingana na malaika wa mbinguni. Hivyo, kuhamishwa ghafla kwa Mheshimiwa Kandoro toka jijini hapa na kwenda Mwanza, kunadhihirisha wazi kuwa hakuwa mtu wa kubabaisha tu kutokana na mabadiliko aliyoyafanya katika mji huu ukilinganisha na awali. Kila kiongozi aliyepita alifanya mabadiliko yake kwa wakati wake.

Hivyo amehamishiwa jijini Mwanza pia, kuleta mabadiliko ya kiuchumi katika taswira ya jiji pamoja na wakazi wake kwa ujumla. Tunakutakia kila la kheri huko uendako mzee wetu Abbas Kandoro, na karibu jijini Dar es Salaam Mheshimiwa William Lukuvi, na hizi ndizo changamoto zetu..


Abbas Kandoro, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam

Monday, April 13, 2009

Ushindani wa kibiashara unaposhika hatamu

Nilishazoea kuona 'Mteja kwetu ni mfalme' katika hoteli,maduka makubwa na kadhalika. Lakini hili la kwenye vituo vya mafuta sasa inaonyesha ni namna gani dhana ya ushindani katika biashara inavyoanza kuchukua nafasi yake.

Sifahamu kama hiki ni kituo cha mzawa ama mgeni. Lakini yote tisa, kumi ni kufunguliwa kwa milango ya kibiashara Afrika Mashariki ambapo sasa tunaanza kuona uwepo wa baadhi ya makampuni mbalimbali ya kigeni yakishika kasi katika sekta ya biashara hapa nchini.

Nchini Kenya kuna desturi ya kunyenyekea mteja zaidi ukilinganisha na kwetu (Tanzania). Sasa sijui ni utamaduni wao ama ni elimu zaidi ya biashara. Wasiwasi wangu ni kufunikwa kwa kampuni za kizalendo na wageni hawa kwa sababu tu ya unyenyekevu na nidhamu zao kwa wateja.

Changamoto yangu kwa kampuni za wazawa, kubadili mitazamo na fikra za kibiashara kulingana na wakati uliopo sasa.


Mpitanjia akipita jirani na bango la kituo cha mafuta lililo na ujumbe wa kuvutia mteja wa bidhaa hiyo..

Friday, April 10, 2009

Wakristo nchini watekeleza Ibada ya Ijumaa Kuu leo

Waumini wa dini ya Kikristo nchini na duniani kote leo wametekeleza Ibada ya Ijumaa kuu ya kumbukumbu ya kufa kwa Yesu Kristo msalabani kwa mujibu wa imani yao. Kwa hapa jijini ibada hiyo imefanyika katika makanisa mbalimbali yakiwemo Kanisa Kuu la Mt. Joseph, Kanisa la Azania Front pamoja na makanisa mbalimbali.

Ibada hiyo iliambatana na maigizo ya mateso ya Yesu Kristo, kwa mujibu wa imani ya waumini hao.



Vijana wa kanisa la Azania Front la jijini Dar es Salaam wakiigiza mateso ya Yesu Kristo, ikiwa ni moja ya Ibada ya Ijumaa Kuu iliyofanyika leo nchini kote na dunia nzima.

Meli ya Mv. Seagull mwendo mdundo

Wiki mbili baada ya Mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa majini na nchi kavu Tanzania (SUMATRA) kusitisha safari za Meli ya Mv. Seagull baada ya kugonga gati la bandari ya bongo, meli hiyo sasa imerejea ulingoni ikiwa na nguvu mpya, ari mpya na kasi mpya baada ya kufanyiwa matengenezo ya kufa mtu.

Kwa mujibu wa mdodosaji wa PONSOR aliyezuru eneo hilo la bandari muhimu ya Da'slam amesema aliiona meli hiyo ikila vichwa (abira) kama kawaida huku sehemu ya mbele iliyokuwa imebonyea ikiwa ipo shwari.

Thursday, April 9, 2009

Prisons na JKT Ruvu nguvu sawa

Timu za Prisons ya Mbeya na JKT Ruvu ya Mkoa wa Pwani leo zimetoka suluhu ya 1-1 katika mchuano wa ligi kuu ya Tanzania Bara uliofanyika uwanja wa Uhuru, jijini hapa.

Wednesday, April 8, 2009

Dah! Dar noma... mvua ya nusu saa tu Town hakufai






Picha za matukio mbalimbali ya mvua zilizonyesha leo jijini Dar.

DECI wakomaa kinoma



Katika hali ya kushangaza na kuonyesha kukomaa kihuduma zaidi, Jumuiya ya Maendeleo ya Wajasiriamali (DECI), wameikomalia Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kuwa kamwe hawapo tayari kuona inaifungia jumuiya hiyo kuendelea na huduma zake.

Akizungumza katika Mkutano wa hadhara na wanachama wa Jumuiya hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya DECI, Askofu Bartholomew Sheggah amesema kuwa jumuiya yake haiwezi kuacha kuendelea kutoa huduma ya kuwasaidia wananchi walo na hali ya chini kwani kwa kufanya hivyo watakuwa wamekiuka malengo ya Rais Jakaya Kikwete ya 'Maisha bora kwa Kila Mtanzania'

"Wanaotaka Jumuiya yetu ifungiwe hao wana nia mbaya na hawataki wananchi wajikwamue katika hali ngumu ya maisha. Sisi tunatimiza ahadi ya Rais Jakaya Kikwete ya 'Maisha Bora kwa Kila Mtanzania'." Alisema.

Mkutano huo uliofurika maelfu ya wanachama hao ulikuwa na lengo la kutolea ufafanuzi wa taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kuhusu kusimamishwa kwa jumuiya hiyo kutokana na madai kuwa haitambuliki kisheria.

Friday, April 3, 2009

Kili Music Awards: Patakuwa hapatoshi!

Kesho ni kesho asemae leo ni muongo. lile shindano kubwa hapa nchini la tuzo za muziki za kilimanjaro lililokuwa linasubiriwa kwa hamu, limefikia patamu.

Leo nilitembelea katika ukumbi wa Diamond Jubilee ambako ndiko kunatarajiwa kufanyika kwa shindano hilo, na nikajionea namna mafundi wakiwa katika hatua za mwisho mwisho za ujenzi wa jukwaa baab kubwa litakalotumika na wasanii wetu hapo kesho.

Bila shaka washabiki wa mambo ya burudani hasa za muziki watakuwa wamejipanga vilivyo kushuhudia shindano hilo. Labda kwa kuwakumbushia viingilio katika tuzo hizo ni shs 50,000/ kwa vip na shs 20,000/ kawaida.

Thursday, April 2, 2009

Tanzania yapata wataalamu wa Upasuaji Ubongo

Tanzania na Madaktari wa Afrika leo zimetiliana saini mkataba wa mpango endelevu wa upasuaji wa ubongo pamoja na uti wa mgongo. Akizungumza baada ya utilianaji saini mkataba huo, Katibu Mkuu wa wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Bi. Blandina Nyoni amesema kuwa madaktari hao watasaidia kupunguza tatizo la uhaba wa madaktari wa fani hiyo.